Ulaji wa Lishe Bora katika Kipindi Chote cha Maisha
Wataalamu wa Afya wanasema kuwa, awamu mbalimbali za maisha zinahitajia ulaji wa chakula wa aina tofauti. Iwapo wewe ni mtoto, mwili wako unahitaji virutubishi ili kusaidia ukuaji wa mwili, kama ni kijana mwili wako una mahitaji maalumu unayoyahitajia kudhamini makuzi ya kiafya ya mwili wako wakati wa utu uzima na wakati unapokuwa mtu mzima unahitaji kuwa na uzito uliolingana na mwili wa wastani.
Tukiangalia katika upande wa Akina mama wajawazito na wale wanaonyonyesha nao pia wana vyakula vyao maalumu wanavyohitajia tofauti kabisa na wanawake wengine. Uchunguzi wa kitiba uliofanywa unaonyesha kuwa, hali ya kiafya ya mama mjazito huwa na athari mbalimbali kwa mtoto atakayezaliwa. Vile vile kuna ushahidi mkubwa kuwa magonjwa sugu ya watu wazima huanzia wakati mtoto bado akiwa tumboni mwa mama yake akiwa katika hali ya kiluilui au (foetus). Kwa hivyo akina mama wajawazito wanashauriwa kuzingatia vyakula wanavyokula kabla na baada ya kushika mimba. Sasa tuangalie athari za chakula kwa afya ya mtoto na virutubisho vinavyopaswa kujumuishwa katika mlo wa mama mjamzito. Chakula cha mama mjamzito kinaweza kuwa na athari kubwa muhimu kwa afya ya watoto kwa miaka mingi baada ya kuzaliwa. Miaka kadhaa ya hivi karibuni, Jarida la Masuala ya Lishe la Uingereza la Prestigious lilichapisha makala tatu kuhusu athari za lishe ya mama mjamzito kwa afya na ukuaji wa kiakili wa mtoto ambaye bado hajazaliwa. Wengi wanafahamu kuwa akina mama wajawazito wanapaswa kula chakula chenye virutubisho vyote vinavyohitajika ili kuhakikisha kuwa watoto wao watakaowazaa wamerutibika vya kutosha wakati wakiwa kwenye fuko la uzazi. Hata hivyo, kile ambacho hatukubaliani nacho hivi sasa ni kwamba chakula cha mama mwenye mimba kinaweza kuwa na taathira chanya kwa afya ya watoto kwa muda wa miaka mingi, baada ya kuzaliwa. Hivi sasa imethibitika kuwa kile kinacholiwa na akina mama wakati wa ujauzito, chakula ambacho kitakuwa kimejumuisha virutubisho vyote vinavyotakiwa, kinaweza kuwafanya watoto wao watakaozaliwa kuwa werevu zaidi. Kwani wataalamu wa afya wanasema kuwa hivi sasa wanaweza kuandaa kizazi kipya cha watoto werevu kwa kula chakula kinachotakikana wakati wa ujauzito. Akina mama wajawazito ambao katika kipindi cha ujauzito hawakupata lishe bora isiyo na mada za protini, nishati, madini na vitamini kwa ujumla huzaa watoto walio na uzito wa chini. Aidha watoto hao huwa na uwezekano mkubwa wa kukumbuwa na magonjwa ya kisukari katika kipindi cha utu uzima.
Wapenzi wasikilizaji baada ya kufahamu umuhimu wa kula lishe bora kwa mama mjamzito na athari zake chanya kwa mtoto atakayezaliwa, sasa tuangalie hatari ya unywaji pombe kwa akinamama wajawazito. Watu wengi wanafahamu madhara yanayotokana na utumiaji wa madawa ya kulevya na ya kawaida pamoja na uvutaji sigara wakati wa ujauzito, lakini wanawake wengi hawana ufahamu wa kutosha kuhusu madhara yanayosababishwa na unywaji pombe wakati wa ujauzito. Utasikia mume au ndugu, jamaa na marafiki wakimshawishi mama mjamzito kwa maneno kama vile" hebu pata kinywaji, kitakuburidisha, kunywa mvinyo kidogo tusherehekee mimba yako. Chupa moja haiwezi kukuathiri bali itakusisimua tu, Hebu tusherehekee sikukuu" n.k. Nadhani wengi tumewahi kusikia maneno kama haya na ushauri usiofaa ambao hauna faida yoyote ghairi ya kuandaa madhara kwa mtoto atakayezaliwa.
Athari za pombe kwa mtoto ambaye bado hajazaliwa:
Unywaji pombe wa aina zozote wakati mama akiwa na mimba huwa na madhara tofauti kwa mtoto aliye tumboni mwake, kuanzia zile za wastani hadi kubwa. Kumbuka kuwa mama anapokunywa pombe mtoto naye hunywa pia. Kuna madhara makuu matatu yanayoweza kumsibu mtoto ambaye bado hajazaliwa iwapo mama yake alikuwa akinywa pombe wakati wa ujauzito. Mosi, ni kuweko hatari kubwa ya kutoka mimba au kuzaliwa mtoto kabla ya miezi tisa, pili, chembe za mwili za mtoto aliye tumboni zinaweza kuathiriwa au anaweza kuwa na uzito mdogo na kuzaliwa akiwa na ulemavu zaidi ya mmoja., tatu, chembe za ubongo wa mtoto huyo zinaweza kuharibiwa na pombe na mtoto kuzaliwa akiwa na matatizo ambayo kitaalamu hujulikana kama Foetal alcohol syndrome. Miongoni mwa madhara yanayoweza kumpata mtoto ni kama vile kuzaliwa akiwa na ulemabu wa kimwili na kiakili. Kwa upande wa kimwili, mtoto huweza kuathiriwa na mtindio wa ubongo au brain retardation, mtoto anaweza kuzaliwa akiwa na kichwa kidogo sana, na uso wake kuwa na mwanya mkubwa baina ya pua na mdomo. Kwa upande wa macho, wengine huzaliwa wakiwa na matatizo ya kuona, masikio hushambuliwa na baadhi ya magonjwa, n.k.. Na tukitazama upande wa ukuaji wa kimaanawi wa mtoto, kuna mambo kadha wa kadha ambayo mama anaweza kuyafanya ili kuandaa misingi bora ya kuwa Muislamu mwema. Maimamu watukufu wametuambia kuwa, mama mjamzito anapasa daima kuwa katika hali ya wudhu. Hii ni kwa sababu Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma anapendelea kumuona mja wake akiwa katika wudhu huku malaika wakimzunguka. Hivyo mama hushauriwa kujiepusha na kutenda dhambi, kwa sababu jambo hilo litakuwa na athari ya moja kwa moja kwa shakhsiya ya mtoto. Kwa hivyo ni jambo lenye umuhimu kwa akina mama kuwaandalia watoto wetu mwanzo mzuri wa makuzi bora tangu wakiwa tumboni.
Na sasa hebu tuangalie jinsi unene unavyosababisha hatari kubwa ya saratani ya matiti kwa wanawake. Wanawake wanaoongezeka uzito kupita kiasi katika utu uzima, wanakabiliwa na hatari kubwa na ya muda mrefu ya kukumbwa na saratani za matiti. Uchunguzi uliofanywa unaonyesha kuwa, uzito na kansa ya matiti vinaweza kuwa na uhusiano wa karibu. Utafiti uliofanywa kwa akinamama zaidi ya elfu 44 nchini Marekani umeonyesha kuwa, kadiri mwanamke anavyozidi kunenepa, ndivyo anavyozidi kujiweka katika hatari ya kukumbwa na kansa mbalimbali, tena katika hatua zake zote. Hatari ya saratani ya matiti imehusishwa na ongezeko la viwango vya hormone ya estrogen na tishu za mafuta zinazozalisha hormone hiyo. Hivyo basi, akina mama wanashauriwa kuboresha uzito wa mwili kwa kufuata misingi ya afya katika kipindi chote cha utu uzima. Je unafahamu kuwa kansa ya matiti inashika nafasi ya pili kwa kusababisha vifo miongoni mwa wanawake wa Marekani ikifuatiwa na saratani ya mapafu?
 
Top