SERIKALI mkoani Kilimanjaro imesema magonjwa  ya minyooo na kichocho ni tishio kwa afya ambapo mwaka jana pekee wagonjwa 57,014 waliofika katika vituo vya afya mkoani humo waligundulika kuugua magonjwa hayo.

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, aliyasema hayo wakati akifungua warsha ya uhamasishaji juu ya magonjwa yasiyopewa kipaumbele (NTD) kwa wakurugenzi na wenyeviti wa halmashauri, wataalamu wa afya na
elimu wa wilaya za mkoa huo.

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhandisi Alfred Shayo, alisema magonjwa ya minyoo na kichocho yanaongoza kwa kuathiri afya za wakazi wengi kutokana na kutochukua tahadhari.

Alisema Wilaya ya Hai inaongoza kwa wagonjwa 12,012 wa minyooo.

“Rombo inashika nafasi ya pili ya wagonjwa 10,753 waliotambulika, kati yake wagonjwa 1,445 waligundulika kuwa na kichocho na wilaya ya Same ilikuwa na wagonjwa 529 na Manispaa ya Moshi iliyokuwa na wagonjwa 359."

Mhandisi Shayo alisema magonjwa yasiyopewa kipaumbele ni magonjwa ambayo yanaathiri jamii ya watu wenye kipato cha chini wanaoishi katika maeneo duni ambayo upatikanaji wa huduma za afya na maji safi na salama ni mgumu.

Aliyataja magonjwa mengine kuwa ni pamoja na matende, mabusha, usubi, trakoma, minyoo ya tumbo, homa ya malale, kichaa cha mbwa, tauni na tegu ambapo alisema athari za magonjwa hayo yasipotibiwa mapema ni pamoja na saratani ya kibofu cha mkojo, ugonjwa wa ini, upofu, utumbo kujifunga pamoja na dalili za kifafa.
 
Top