Uhusiano wa Vyakula na Afya ZetuAhlan wasahlan wapenzi wasikilizaji ni matumaini yangu kuwa hamjambo na karibuni kujiunga nami katika kipindi kingine cha Ijue Afya Yako. Kipindi ambacho lengo lake kuu ni kujadili masuala mbalimbali yatakayotupa ufahamu kwa ajili ya kuziimarisha afya zetu na kulinda miili yetu Kama mnakumbuka katika kipindi chetu kilichopita tulibainisha masuala tofauti na jinsi yanavyoathiri afya zetu. Masuala hayo tulisema ni kama vile mazingira yanayotuzunguka, watu tunaoishi nao, jinsia zetu, jenetiki, mila na desturi na hata idadi ya vituo vya afya na hospitali katika jamii zetu. Pia tulizungumzia lishe bora na mlo uliokamilika na tukamalizia kwa kuwabainishia wasikilizaji wetu vidokezo muhimu au healthy tips zinazotuelekeza namna ya kula vyema ili kulinda na kuziimarisha afya zetu. Katika kipindi chetu cha leo tutazungumzia uhusiano uliopo kati ya vyakula, afya na magonjwa.
Kama ambavyo tumezoa kusikia katika jamii zetu kuwa karoti husaidia kuona vizuri, spinachi huimarisha misuli, maziwa hujenga mifupa na kadhalika, hayo yote yanaonesha uhusiano uliopo kati ya vyakula na afya zetu. Kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya vyakula tunavyokula, afya zetu na maradhi. Hii ni kwa sababu vyakula tunavyokula vinaweza kuwa ni lishe bora kwa miili yetu au kinyume chake. Vilevile kiwango cha chakula tunachokula na kuupatia mwili wetu pia kina taathira ya moja kwa moja kwa afya zetu.  Kuwa na ufahamu kuhusiana na chakula tunachokula, lishe na afya kunatupa uwezo wa kuweza kuchagua chakula cha aina gani tule na kwa kiwango gani suala ambalo kwa ujumla huusaidia moja kwa moja kuimarisha afya zetu, kuiepusha miili yetu na baadhi ya maradhi na hata kutibu baadhi ya magojwa tunayopata. Baadhi ya magonjwa kama matatizo ya moyo na mishipa ya damu, asthma, kisukari na hata kensa pia yanaweza kuwa na uhusiano, ambao ni mabadiliko yanayosababishwa na uvimbe wa muda mrefu mwilini au chronic inflammatory reaction, mabadiliko ambayo huanzia katika tishu ya mafuta. Wataalamu wanasema lishe ina taathira kubwa katika suala hilo. Tabia nzuri au mbaya ya kula, huweza kumfanya mtu kuwa mnene na mafuta ya ziada mwilini mwake hugeuka na kuwa kama uvimbe wa muda mrefu, suala ambalo huweza kusababisha maradhi kwenye moyo na mishipa ya damu, asthma, kisukari na hata kensa. Kwa kula lishe bora na salama pamoja na kujiepusha na unene wa kupindukia tunaweza kuusaidia mwili kutokuwa na mafuta mengi jambo ambalo huzuia baadhi ya maradhi kama hayo tuliyoyataja. Uhusiano kati ya chakula na afya umeleta changamoto kubwa katika masuala ya afya na kumefanyika tafiti nyingi katika uwanja huo. Kwa mfano utafiti uliofanywa na Martha Clare Morris na timu yake huko Chicago Marekani kuhusiana na uhusiano uliopo kati ya ugonjwa wa usahaulifu wa Alzheimer, unaweza kukufanya hata wewe ndugu msikilizaji kujiuliza mara mbili kabla ya kuamua chakula utakachokula. Watafiti hao kwanza wamegundua kuwa, vyakula vyenye vitamin E vinahusiana moja kwa moja na kupunguza uwezekano wa kupata ugonjwa wa Alzheimer. Vyakula hivyo ni pamoja na nafaka zilizorutubishwa, mboga za rangi kijani, tikiti maji, mbegu (seeds) mbalimbali na jamii ya karanga. Pia wamefahamu kuwa, watu wanaokula samaki kwa wingi kwa uchache mara moja kwa wiki, huwa wamepunguza kwa asilimia 60 hatari ya kupatwa na gonjwa hilo la usahaulifu au Alzheimer kuliko wale ambao hawali kabisa samaki au hula samaki mara chache. Sio vibaya kutambua kwamba, ugonjwa huo huwapata karibu  watu milioni 24 duniani kila mwaka hasa watu watu wazee.
Hebu sasa tuangalie uhusiano uliopo kati ya ugonjwa wa moyo na chakula.  Baadhi ya vyakula vyenye mafuta mengi husababisha kwa kiasi kikubwa maradhi ya moyo kwani kiwango kikubwa cha mafuta aina ya trans fats yaliyopo kwenye vyakula hivyo kwa mfano vyakula vya fast food, yanaweza kuziba mishipa ya damu na baada ya muda kuongeza kiwango chakolestero mwilini. Suala hilo katika miaka ya hivi karibuni limeleta wasiwasi mkubwa hasa kutokana na kuongezeka idadi ya vijana wenye umri mdogo wenye unene wa kupindukia, hali inayosababishwa na kula vyakula vyenye mafuta vinavyopikwa majiani au nje ya nyumba vinavyojulikana kimombo kama fast food. Vyakula hivyo ni kama chips au viazi vya kukaanga, kuku wa kukaanga, samaki wa kukaanga, bisikuti, piza, keki  na vinginevyo.  Mafuta ya aina hiyo hutokana na mafuta ya majimaji na yale ya samli na huweza kusababisha magonjwa ya moyo. Uchunguzi uliofanywa na wataalamu wa afya ya Jamii wa Chuo Kikuu cha Havard nchini Marekani na kuchapishwa katika Jarida la Jumuiya ya Magonjwa ya Moyo ya Marekani umeonyesha kuwa, aina ya mafuta ya trans fats huongeza mara tatu magonjwa ya moyo kwa wanawake. Inafaa kukumbusha hapa kwamba ugonjwa wa moyo ni ugonjwa unaoongoza kwa kuua duniani. Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani WHO,  ugonjwa wa moyo na mishipa ya damu husababisha asilimia 63 ya vifo vyote vinavyotokea dunia,  huku tafiti zikionyesha kwamba kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya vyakula vyenye mafuta mengi na ongezeko la maradhi ya moyo.
Kilichopo hewani mpenzi msikilizaji ni kipindi cha 'Ijuwe Afya Yako' kinachowajia kupitia idhaa ya kiswahili Sauti ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Kama tulivyoahidi huko nyuma katika kipidi hiki pia tutakuwa tukizungumzia baadhi ya tafiti na chunguzi mbalimbali zilizofanywa kuhusiana na masuala ya afya.
Hivi karibuni uchunguzi mpya umeonyesha kwamba kula zabibu au vyakula vyenye zabibu ndani yake hupunguza shinikizo la damu, husaidia moyo kufanya kazi zake vyema na kupunguza hatari ya kupatwa na ugonjwa wa moyo. Kwa mujibu wa uchunguzi huo uliotangazwa kenye mkutano wa Majaribio ya Biolojia huko California, zabibi zina uwezo wa kupunguza shinikio la damu, husaidia mwili uweze kuvumilia sukari (glucose tolerance) na kupunguza kiwango cha mafuta aina ya triglycerides mwilini ambayo ni chanzo cha matatizo ya moyo. Wataalamu wanasema zabibu pia zinaweza kupunguza uvimbe, uharibivu unaotokana na free radicals zinazozalishwa mwilini, na shinikizo la moyo. Hayo yote yakitokana na mada zijulikanazo kama phytochemicals zilizoko kwenye matunda ya zabibu. Matunda hayo huzuia tatizo linalojulikana kama Metabolic Syndrome. Metabolic Syndrome ni mchanganyiko wa matatizo ya kitiba yanayoongeza uwezekano wa kupatwa na maradhi ya mishipa ya damu pamoja na kisukari. Hivyo wataalamu wanatushauri tule zabibi au kuongeza zabibu katika vyakula tunavyokula kila siku, ili tujikinge na ugonjwa huo, maradhi ya moyo na kisukari aina ya pili (type 2 diabates). Haya shime wapenzi wasilizaji tule zabibu kwa ajili ya afya zetu.Tumetahadharishwa kwamba kulala chini ya masaa 6 kila usiku kunaweza kusababisha mtu afe mapema. Wataaalamu wamesema kwamba watu ambao kwa kawaida huwa wanalala masaa hayo machache wengi wao hupatwa na vifo vya mapema kwa asilimia 12 zaidi ya wale wanaolala kawaida kwa masaa 8, vifo ambavyo hutokea katika umri wa baada ya miaka 25. Pia imeonyeshwa kwamba kulala kwa zaidi ya masaa 9 pia kunapelekea vifo vya mapema ingawa kulala huko kunaweza kukawa na uhusiano na matatizo ya kiafya. Utafiti huo umetolewa kwa kuchunguzwa uhusiano uliopo kati ya kifo na usingizi kwa kutegemea chunguzi 16 zilizofanywa kwa kuwahusisha watu milioni 1 na nusu katika nchi za Uingereza, Marekani , Ulaya na Mashariki mwa Asia. Profesa Francesco Cappiccio aliyeongoza utafiti huo wa Chuo Kikuu cha Warwick cha Uingereza anasema, jamii za  sasa zilizoendelea zimekuwa taratibu zikipunguza muda wa kulala, na tatizo hili linawapata sana watu wanaofanya kazi masaa mengi. Amesema suala hili linaonyesha kwamba hayo yote yanatokana na mashinikizo ya kimaisha yanayowapelekea watu wafanye kazi masaa mengi na kuchukua shifti nyingi za kazi. Amesema kwamba, kuporomoka kwa afya kunaambatana na kulala masaa mengi zaidi. Usingizi ni kama karatasi ya litmus inayoonyesha afya na hali ya mwili na akili ya mtu kwani usingizi unaathiriwa na magonjwa na hali mbalimbali ukiwemo msongo wa mawazo au depression, anasema mtaalamu huyo. Tunashauriwa tusilale masaa machache wala mengi kupita kiasi bali tulale kwa masaa ya wastani ambayo ni masaa 8.
Na utafiti unaotuhitimishia kipindi chetu cha afya leo ni ule unaosema kwamba, kuna uhusiano kati ya kucheka na kuishi maisha marefu. Utafiti huo uliochapishwa katika Jarida la Saikolojia la Sayansi umeonyesha kwamba, watu wenye tabasamu pana linalojulikana kama 'Dunchenne smile', huishi maisha marefu. Ernest L. Abel aliyeongoza utafiti huo amesema kwamba, watu ambao wanaonyesha hisia zao na kuziakisi kwa tabasamu pana, kimsingi huwa ni watu wenye furaha zaidi kuliko wale wenye kutabasamu kidogo. Hivyo watu hao hufaidika na suala hilo na kwa kawaida huishi maisha marefu. Wataalamu wanasema kwamba watu wenye kutabasamu sana kwa kawaida huwa wana furaha, shaksia madhubuti, ndoa zao hudumu zaidi, wana ufahamu mzuri zaidi wa mambo na huwa na maingiliano mazuri na watu wengine.
Na kufikia hapo wapenzi wasikilizaji hatuna la ziada.
 
Top